Bosi Simba SC aahidi kupunguza zaidi nyota wao

KANDANDA Bosi Simba SC aahidi kupunguza zaidi nyota wao

Zahoro Juma • 16:00 - 22.01.2024

Kauli hiyo imekuja siku moja baada ya klabu hiyo kufanya Mkutano Mkuu wa kila mwaka ambapo baadhi ya wanachama walionesha kutofurahia usajili wa sasa

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Klabu ya Simba, Salim Muhene 'Try Again', amesema licha ya kuwakata baadhi ya nyota wao katika dirisha dogo la usajili lililopita lakini wanatarajia kupiga panga kubwa zaidi katika usajili ujao mwishoni mwa msimu.

Try Again amesema panga hilo linatokana na maelekezo ya Kocha Mkuu wa Simba, Abdelhak Benchikha, ambaye inadaiwa anahusika na maamuzi yote ya usajili kwa asilimia 100.

Akizungumza na Pulse Sports, Try Again, amesema kwasasa Benchikha yupo katika hatua za kukijenga kikosi chake, hivyo wao kama viongozi hawana budi kutimiza matakwa ya mwalimu.

"Sisi kama viongozi tumefanya kazi ambayo tumetakiwa kuifanya na benchi la ufundi, wachezaji wote walioingia na waliotoka ni kutokana na mapendekezo ya Kocha Benchikha," amesema.

Aidha Try Again amewataka wachezaji wote wapya na wa zamani kuendelea kutumia vizuri nafasi wanazopewa uwanjani kwani hakutakuwa na huruma wakati wakufanya maamuzi ifikapo mwisho wa msimu.

Amesema hakuna jina litakaloonewa haya wala hawataangalia kuwa pengine mchezaji fulani ni kipenzi cha mashabiki hivyo waweze kumbakisha kwenye kikosi chao.

"Kinachotakiwa ni wachezaji kujituma pindi wanapopewa nafasi lakini pia mazoezini, kwenye dirisha hili kuna wachezaji tulipanga kuwaacha lakini jitihada zao hasa katika michuano ya Mapinduzi Cup zimefanya tumebadili mawazo," amesema.

Katika dirisha la usajili liliofungwa wiki iliyopita, Simba ilitangaza kuachana na wachezaji sita wakikosi cha kwanza ambao ni Jean Baleke, Moses Phiri, Nassoro Kapama, Shaban Chilunda, Jimmyson Mwanuke na Mohamed Mussa.

Wakati wakiachana na wachezaji hao, pia walitangaza nyota wapya sita kutoka ndani na nje ambao ni Saleh Karabaka, Ladack Chasambi, Edwin Balua wote kutoka Tanzania. Wengine ni Pa Omar Jobe (Gambia), Babacar Sarr (Senegal) na Freddy Michael Koublan (Ivory Coast).

Tags: