Bacca asaini mkataba wa miaka nne kubaki Yanga SC

KANDANDA Bacca asaini mkataba wa miaka nne kubaki Yanga SC

Zahoro Mlanzi • 19:45 - 29.11.2023

Beki huyo hivi karibuni amepewa heshima na klabu hiyo kwa mchezo wao wa Jumamosi dhidi ya Al Ahly ya Misri wa hatua ya makundi Ligi ya Mabingwa Afrika kuuita 'Bacca Day'

Beki wa kisiki, Ibrahim Abdulla 'Bacca', ameongeza mkataba wa miaka minne kuendelea kuitumikia timu ya Yanga SC hadi mwaka 2027.

Bacca ambaye hivi karibuni amepewa heshima kubwa katika mchezo ujao dhidi ya Al Ahly ya Misri kupewa jina lake 'Bacca Day', pia ni mchezaji tegemeo kwa timu ya Taifa 'Taifa Stars'.

Nyota huyo wa zamani wa KMKM ya visiwani Zanzibar, amekuwa nguzo muhimu kwa timu hizo kutokana na ubora anaouonesha katika mechi mbalimbali anazocheza.

Mkataba huo wa miaka minne, unamfanya kufikia rekodi aliyoweka nyota wa zamani wa timu hiyo, Feisal Salum 'Fei Toto' ambaye kwa sasa anaichezea Azam FC, kusaini muda mrefu zaidi kwa soka la Tanzania.

Fei Toto alisaini mkataba huo mwaka 2020 ambapo kama angekuwepo hadi leo basi mkataba huo ulikuwa unaisha mwishoni wa msimu huu.

Mbali na wachezaji hao, lakini mkataba kipa, Ramadhani Kabwili wa miaka mitano aliosaini mwaka 2017 bado unasalia kuwa ndio mkataba mrefu zaidi ndani ya klabu hiyo.

Akizungumza na Pulse Sports, Rais wa Yanga, Injinia Hersi Said, amesema wameamua kumuongeza mkataba mchezaji huyo kutokana na uwezo wake ambao amekuwa anaonesha kwenye michezo mbalimbali.

"Tumeamua kumpa mkataba mrefu na wenye thamani kubwa tofauti na ule wa mwanzo kwasababu ya uwezo wake na kujituma kwake uwanjani," amesema.

Mkataba wa Yanga na Bacca ulikuwa unaelekea ukingoni kwani alisajiliwa katikati ya msimu wa mwaka 2021 na aliingia mkataba wa miaka miwili kipindi hicho.

Mbali na hilo, Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), limempanga, Mwamuzi Abdel Azia Mohamed Bouh kuwa ndio mwamuzi wa mchezo kati ya Yanga na Al Ahly utakaopigwa Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Tags: