Tanzania yaingiza timu mbili makundi CAFCL

© Kwa Hisani

KANDANDA Tanzania yaingiza timu mbili makundi CAFCL

Zahoro Mlanzi • 12:30 - 02.10.2023

Yanga jana imefuzu hatua hiyo kwa mara ya kwanza ikipita miaka 25 baada ya kuibuka na ushindi wa jumla wa mabao 3-0 dhidi ya Al-Merreikh ya Sudan.

Ni historia! Ndivyo unavyoweza kusema baada ya Tanzania kwa mara ya kwanza kuingiza timu mbili hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) baada ya timu ya Simba SC kuifuata Yanga katika hatua hiyo.

Yanga jana imefuzu hatua hiyo kwa mara ya kwanza ikipita miaka 25 baada ya kuibuka na ushindi wa jumla wa mabao 3-0 dhidi ya Al-Merreikh ya Sudan.

Kwa upande wa Simba, ambayo kucheza hatua hiyo si jambo geni kwani katika misimu zaidi ya minne mfululizo imekuwa ikifuzu, imetinga baada ya kuwa na faida ya bao la ugenini ikitoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Power Dynamos ya Zambia katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.

Katika mchezo wa mkondo wa kwanza uliopigwa mjini Ndola, Zambia, Simba ilipata sare ya mabao 2-2 hivyo kuwa na mtaji wa bao moja la ugenini.

Katika mchezo huo, Dynamos ndio imekuwa ya kwanza kufunga bao dakika ya 16 kupitia kwa Andy Boyeli, aliyefumua shuti nje ya eneo la hatari na kujaa moja kwa moja wavuni huku kipa, Mmisri Ayoub Lakred akiruka bila mafanikio.

Boyeli ambaye msimu uliopita ndiye alikuwa Mchezaji na Mfungaji Bora wa Ligi Kuu ya Zambia, amefunga bao hilo baada ya kupokea pasi iliyopigwa na beki wa kulia, Kondwani Chiboni.

Pamoja na kufungwa bao hilo, Simba ndio imetawala mchezo huku ikipata nafasi dakika ya 36 kupitia kwa Jean Baleke aliyekuwa ndani ya eneo la hatari lakini shuti alilopiga lilitua mikononi mwa kipa, Willard Mwanza.

Kipindi cha pili, Simba imeongeza kasi hasa baada ya kuona Dynamos ikicheza na watu wengi zaidi nyuma ya mpira huku ikifanya mashambulizi ya kushtukiza.

Presha hiyo imezaa matunda katika dakika ya 68 baada ya nahodha wa Simba, John Bocco aliyeingia badala ya Baleke kupiga shuti ndani ya eneo la hatari na beki, Chiboni kuujaza wavuni akiwa katika harakati za kuokoa.

Pamoja na bao hilo, Simba bado imeendeleza mashambulizi langoni mwa Dynamos ambapo kama Bocco na Saido Ntibazonkiza wangekuwa makini wangeifungia mabao zaidi timu yao.

Hata hivyo, Simba imetinga hatua hiyo lakini mashabiki waliokuwepo uwanjani Chamazi Complex, nyuso zao zilionesha kutoridhishwa na matokeo hayo licha ya kufuzu hatua ya ushindi.

Mmojawapo, Kessy Mdende amenukuliwa na Pulsesports akisema:"Tumeshinda lakini timu haina kiwango kizuri, tupo katika michuano ya African Super League na tutacheza na Al Ahly kama kocha asipojipanga vizuri tutafungwa mabao mengi zaidi.