Kapombe 'alia' kutoka sare na Azam FC

KANDANDA Kapombe 'alia' kutoka sare na Azam FC

Zahoro Juma • 14:32 - 10.02.2024

Ni baada ya timu yake ya Simba SC kusawazisha bao dakika za lala salama.

Beki mkongwe wa timu ya Simba SC, Shomari Kapombe, amesema imewaumiza kupata sare dhidi ya Azam kwasababu walijipanga kuvuna alama tatu kwenye mchezo huo.

Akizungumza mara baada ya mchezo huo uliochezwa jana Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, Kapombe amesema kuruhusu bao la mapema kuliharibu mipango yao.

Amesema Azam waliwapa wakati mgumu hasa pale walipokuwa hawana mpira kwasababu walikuwa wanarudi nyuma wote.

"Azam walitupa mechi ngumu na hasa baada ya kufunga bao mapema, tulijiandaa kushinda lakini hata alama moja sio mbaya," amesema.

Beki huyo mkongwe ndani ya kikosi cha Simba, ameongeza kwa kwasasa akili yao wanahamishia kwa Geita Gold watakaoumana na Jumatatu katika mchezo mwengine wa Ligi Kuu Bara utakaofanyika CCM Kirumba.

Simba sasa imefikisha alama 30 katika nafasi ya tatu ikiwa ni alama saba nyuma ya vinara, Yanga.