Kocha Kitambi atambulishwa rasmi Geita Gold FC

LIGI KUU Kocha Kitambi atambulishwa rasmi Geita Gold FC

Na Zahoro Mlanzi • 19:18 - 21.12.2023

Kocha huyo alitimuliwa wiki iliyopita na Namungo FC ambayo mechi yake ya mwisho aliiongoza kushinda 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar

Uongozi wa timu ya Geita Gold FC, umemtangaza Kocha, Denis Kitambi kuwa kocha mkuu wao akiziba nafasi iliyoachwa wazi na Kocha, Hemed Suleiman 'Morocco' ambaye alidai kuomba kupumzika.

Kitambi anajiunga na Geita akiwa anatokea kwenye kikosi cha Namungo ya mkoani Lindi ambacho alikiongoza katika michezo saba ya Ligi Kuu Bara na kushinda minne, sare mbili na kupoteza mchezo mmoja.

Mchezo wake wa mwisho kuiongoza Namungo ilikuwa ni Desemba 7 ambapo aliwasaidia kushinda 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar.

Kwa mujibu wa taarifa ya timu hiyo waliyoitoa usiku wa kuamkia jana, wameachana na Morocco kwakuwa aliomba muda zaidi wa kufanya kazi zake za usaidizi katika timu ya taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' na sasa wanamkaribisha Kitambi kuanza maisha mapya.

Kikosi cha Geita Gold kinashika nafasi ya 13 kwenye msimamo wa ligi hiyo kikiwa kimevuna alama 13 katika michezo 12 walioshuka dimbani.

Kuondoka kwa Morocco ndani ya Geita kunafanya idadi ya makocha 12 ambao wameachana na timu zao tangu kuanza kwa ligi msimu huu.

Tags: