Simba SC, Azam FC ni mechi ya kisasi leo CCM Kirumba

Winga wa Azam, Abdul Suleiman 'Sopu' (kushoto), akiwania mpira na Sadio Kanoute wa Simba katika moja ya mechi zao

KANDANDA Simba SC, Azam FC ni mechi ya kisasi leo CCM Kirumba

Zahoro Juma • 10:04 - 09.02.2024

Ni timu ambazo zimekuwa zikifanya vizuri katika Ligi Kuu Bara, hivyo mchezo huo utavuta hisia za mashabiki wengi

Ni Mzizima Derby! Ni mechi ambayo imekuwa ikisubiriwa kwa hamu kubwa kati ya wenyeji, timu ya Simba SC ambayo itaumana na Azam FC katika mfululizo wa michezo ya Ligi Kuu Bara.

Mchezo huo utapigwa leo saa 10 jioni kwa saa za Afrika Mashariki na Kati kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza kutokana na Uwanja wa Benjamini Mkapa jijini Dar es Salaam kuwa katika ukarabati.

Awali mchezo huo ulitakiwa kupigwa mwishoni mwa waka jana lakini uliahirishwa kutokana na ugumu wa ratiba kwa Simba ambayo ilikuwa ikicheza michuano ya AFL na Ligi ya Mabingwa Afrika.

Katika mechi mbili za ligi msimu uliopita, Azam iliibuka na ushindi katika mechi moja na mechi nyingine iliisha kwa sare lakini walipokutana katika mchezo wa Azam Sports Federation Cup (ASFC), Simba ilikubali kichapo kingine cha 1-0.

Azam ambao kwa muda mrefu walikuwa vinara wa ligi, kwasasa ipo nafasi ya pili wakiwa na alama 31 na Simba ikishika nafasi ya tatu wakiwa na alama zao 29 huku Yanga ikiwa kileleni kwa alama 37.

Katika mchezo huo, Simba imeongezewa nguvu kwa kurejea kiungo wao, Fabrice Ngoma, ambaye alikosekana katika mechi tatu zilizopita kutokana na kuwa majeruhi.

Simba inaingia katika mchezo huo wakiwa na kumbukumbu ya ushindi katika mechi mbili mfululizo za ligi dhidi ya Mashujaa na Tabora United ambazo zote walicheza ugenini.

Hata hivyo, Azam wao mara ya mwisho kuonekana uwanjani ilikuwa ni Desemba 21 kwenye Uwanja wa Kaitaba, Kagera ambapo waliwafunga wenyeji Kagera Sugar kwa mabao 4-0.

Akizungumzia maandalizi ya kikosi chake kuelekea mchezo huo, Kocha Msaidizi wa Simba, Seleman Matola, amesema wanakwenda kukabiliana na mpinzani mgumu lakini wao wamejiandaa kucheza mechi hiyo kwa ufanisi wa hali ya juu ili kuvuna alama tatu.

"Azam ni timu kubwa hivyo maandalizi yetu yalikuwa katika ukubwa ambao unalingana na mpinzani ambaye tunacheza naye, kwa hakika tunaamini kuwa mchezo huu tunakwenda kufanya vizuri," amesema.

Kwa upande wa Azam, wao watamkosa kiungo wao mkabaji, Sospter Bajana ambaye amerejea na majeraha akitokea Afcon.

Pia watamkosa mshambuliaji wao, Allasane Diao ambaye kwa siku za hivi karibuni alionekana kuimarika kabla ya kuumia katika mechi ya kirafiki dhidi ya KVZ iliyochezwa wiki iliyopita.

Lakini Kocha wao Msaidizi, Bruno Ferry, amesema wamejipanga kuhakikisha wanapata matokeo mazuri licha ya kwamba mchezo utakuwa mgumu.