Kocha Benchikha awatema Bocco, Manula safari ya Botswana

KANDANDA Kocha Benchikha awatema Bocco, Manula safari ya Botswana

Na Zahoro Mlanzi • 11:25 - 01.12.2023

Huo ni mchezo wake wa kwanza utakuwa kwa Kocha huyo tangu ajiunge na Simba SC

Kikosi cha timu ya Simba SC, kimeondoka nchini Tanzania leo alfajiri kwa ajili ya kwenda Botswana katika mchezo wao wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Janweng Galaxy

Timu hiyo imeondoka na wachezaji 20 pamoja na benchi lao la ufundi lote huku ikiwaacha nahodha wa timu hiyo, John Bocco, Kipa Aishi Manula na Shaaban Chilunda.

Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa saa 10 jioni nchini humo kwa saa za Afrika Mashariki na Kati.

Kwa mujibu wa taarifa iliyowekwa katika mtandao wa kijamii wa X wa klabu hiyo, imeonesha orodha ya wachezaji 20 bila ya nyota hao kuwepo.

Taarifa zinaeleza Manula ameachwa kwa sababu aliumia akiwa kwenye majukumu ya timu ya Taifa 'Taifa Stars' wiki iliyopita, lakini Bocco na Chilunda hawapo kwenye mpango wa Benchika katika mechi yake ya kwanza kazini Simba SC.

Ikumbukwe mechi ya kwanza ya Kundi B Ligi ya Mabingwa, Simba ililazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na ASEC Mimosas ya Ivory Coast Uwanja wa Benjamín Mkapa Jijini Dar es Salaam Jumamosi iliyopita.

Na Galaxy yenyewe iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Wydad Casablanca ugenini.

Huo ni mchezo wa kwanza kwa Benchikha tangu arithi mikoba ya Mbrazil, Roberto Oliviera 'Robertinho' aliyetimuliwa mwezi uliopita